27/11/2010 11.23.24


Vijana ni matumaini ya Kanisa na Jamii, wanapaswa kuandaliwa kwa sera na mikakati makini


|

Askofu mkuu Victor Tonye Bakot wa Jimbo kuu la Younde, Cameroon, anawataka wanasiasa na Kanisa kwa ujumla kuhakikisha kwamba, wanaweka mikakati na sera endelevu zitakazowawezesha vijana kushikka atamu katika nyanja mbali mbali za maisha, wakati huu na kwa siku za usoni. Vijana wawezeshwe katika maisha ya kimaadili na utu wema; ili waweze kuwa ni watekelezaji makini, wakiendelea kuwa waaminifu kwa Mungu, Kanisa na Jamii kwa ujumla.
Changamoto hii imetolewa na Askofu mkuu Bakot alipokutana na Rais Paul Biya wa Cameroon, ili kujadiliana kwa pamoja, matukio makuu yaliyoko mbele yao: yaani maandalizi ya Sinodi ya Vijana wa Jimbo kuu la Younde, Cameroon, inayotarajiwa kufanyika mwishoni mwa Mwezi Novemba, 2010, ikiongozwa na mada, Mwelekeo wa Vijana kwa Kanisa na nchi ya Cameroon; leo na kesho yenye matumaini.
Kanisa pia linajiandaa kuadhimisha Jubilee ya miaka mia moja na ishirini tangu waliposikia kwa mara ya kwanza Habari Njema ya wokovu ikitangazwa nchini mwao. Maadhimisho yote haya yanakwenda sanjari na Jubilee ya Miaka hamsini tangu Cameroon ilipojipatia uhuru wake.
Jubilee ya miaka hamsini ya uhuru, iwe ni fursa kwa wananchi wa Cameroon kusali na kutafakari, kuhusu dhamana na huduma ya Kanisa kwa kuendelea kuwa waaminifu kwa Mungu na jirani zao. Ni changamoto kwa wananchi wa Cameroon kuhakikisha kwamba, Mwenyezi Mungu anapewa kipaumbele cha kwanza katika maisha na utume wao.
|