04/11/2010 9.17.36


Familia ni kitovu cha amani na upendo


|

Askofu mkuu Josè De Queioros Alves wa Jimbo kuu la Huambo, Angola, hivi karibuni, amezitaka familia kujenga mazingira yatakayoziwezesha kuendelea kuwa ni wadau wakuu katika kazi ya uumbaji waliyokabidhiwa na Mwenyezi Mungu, kwa kujenga na kudumisha mazingira ya amani na upendo wa dhati.
Askofu De Queiròs Alves ameyasema hayo wakati alipokuwa anazungumza na washiriki wa mkutano wa nne ngazi ya kijimbo, uliokuwa unajadili kuhusu umuhimu wa kudumisha tunu msingi za maisha ya kifamilia. Amewataka wajumbe kufanya tafakari ya kina kuhusu hali halisi ya familia katika ulimwengu mamboleo, ili hatimaye, kujenga mazingira yatakayoharakisha amani, upendo na mshikamano wa dhati, kila mtu akijitahidi kutekeleza wajibu wake, ili kuboresha maisha ya kifamilia.
Hii ndiyo changamoto kubwa inayoendelea kuzikabili familia za kikristo katika ulimwengu mamboleo, ili hatimaye, ziweze kusimama kidete: kulinda na kutetea tunu msingi za kifamilia kwa ajili ya mafao ya Jamii nzima. Ni mwaliko wa kusaidiana ndani ya familia, ili kujenga upendo wa kweli na fadhila nyingine za kikristo. Familia kwa hakika anasema Askofu De Queiròs inapaswa kusimama kidete kulinda zawadi ya maisha dhidi ya utamaduni wa kifo, kwa kutekeleza majukumu yake na hatimaye, kutafuta suluhu ya matatizo wanayokumbana nayo katika mwanga wa Kiinjili.
|