12/10/2010 8.54.57


Mbinu mkakati wa kupambana na baa la njaa, utapiamlo na umaskini duniani!


|

Jumuiya ya Kimataifa kwa muda wa juma zima, kuanzia Jumatatu tarehe 11 hadi 15 Oktoba, 2010 inakutana ili kujadili pamoja na mambo mengine: hali ya usalama wa chakula duniani; athari za kuchechemea kwa uchumi wa kimataifa, changamoto kutoka kwa makampuni ya kigeni yanayowapokonya wananchi maeneo makubwa ya ardhi hasa katika nchi maskini zaidi duniani.
Mashirika makuu ya Umoja wa Mataifa yanayojihusisha na masuala ya chakula na kilimo yanachambua kwa kina hali ya usalama wa chakula duniani, mkutano ambao unatarajiwa kuhitimishwa hapo tarehe 15 Oktoba, katika mkesha wa kilele cha maadhimisho ya Siku ya chakula duniani hapo tarehe 16 Oktoba, 2010.
Kwa mara ya kwanza mkutano huu unahudhuriwa na wajumbe kutoka katika vyama vya kiraia na mashirika yasiyo ya kiserikali, kama sehemu ya mabadiliko makubwa yaliyofanywa kwenye kamati ya kimataifa inayoshughulikia hali ya usalama wa chakula duniani. Lengo ni kuibuka na mbinu mkakati utakaosaidia kupambana na baa la njaa duniani, kwa kuboresha sera za kilimo, ugavi wa misaada ya maendeleo pamoja na kudumisha uhusiano mwema baina ya nchi wanachama.
Mkutano huu unafanyika wakati ambapo bei ya mazao ya nafaka inaendelea kuongezeka maradufu, kama ile iliyojitokeza mwezi Juni, 2008 wakati wa kilele cha kuchechemea kwa uchumi wa kimataifa. Akiwakaribisha wajumbe katika mkutano huu, Dr. Jacque Diouf, mkurugenzi mkuu wa FAO amewakumbusha wajumbe kwamba, changamoto ya usalama wa chakula duniani inahitaji mbinu mkakati wa kimataifa na maeneo husika, ili kupata majibu ya pamoja.
FAO inapenda kuhakikisha kwamba, baa la njaa linatokomezwa duniani kwa kutumia wataalam wake wanaopaswa kushirikiana na wadau wengine katika sekta ya kilimo. Dr. Diouf anasema kwamba, umefika wakati kwa Jumuiya ya Kimataifa kupambana kufa na kupona na baa la njaa, utapiamlo pamoja na umaskini. Hadi sasa kuna jumla ya nchi thelathini ambazo zinakabiliwa na uhaba wa chakula na kwamba, wanahitaji chakula cha msaada. Jumuiya ya Kimataifa inapaswa kujifunga kibwebwe ili kudhibiti kuporomoka kwa tija na uzalishaji katika sekta ya kilimo.
|