01/07/2010 10.08.29


Benedikto XVI aonesha mshikamano wa dhati na waamini nchini Eritrea na Sudan


|

Kardinali Leonardo Sandri, Mwenyekiti wa Baraza la Kipapa kwa ajili ya Makanisa ya Mashariki, tangu tarehe Mosi hadi 6 Julai, 2010 atakuwa na ziara ya kichungaji nchini Eritrea, katika maadhimisho ya Jubilee ya miaka mia moja na hamsini, tangu Mtakatifu Giustino De Jacobis alipofariki dunia.
Kanisa linapenda kuenzi mchango wa Mtakatifu Jacobis, kama muasisi wa Kanisa Katoliki nchini Eritrea. Kardinali Sandri anatembelea Eritrea kwa mwaliko wa Baraza la Maaskofu Katoliki nchini humo na baadaye atapata pia fursa ya kutembelea Sudan, ili kukutana na watu wa Mungu katika eneo hili. Kwa namna ya pekee, ni kutaka kuonesha mshikamano wa dhati kutoka kwa Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita kwa watu wa Mungu nchini Eritrea na Sudan.
Mtakatifu Giustino De Jacobis aliishi kati ya Mwaka 1800 hadi mwaka 1860. Kunako mwaka 1839 aliteuliwa kuwa msimamizi wa kitume Jimboni Eritrea. Mwaka 1849 aliwekwa wakfu kuwa Askofu na mwaka 1975 akatangazwa kuwa Mtakatifu na Baba Mtakatifu Paulo wa sita. Kanisa Katoliki nchini Ethiopia na Eritrea yako chini ya usimamizi wa Baraza la Kipapa kwa ajili ya Makanisa ya Mashariki.
|